NINI CHA KUFAHAMU KUHUSU UGONJWA WA UKOMA

Dr Kuduishe Kisowile

Dr Kuduishe Kisowile

NINI CHA KUFAHAMU KUHUSU UGONJWA WA UKOMA

Tanzania ni kati ya nchi zinazopewa kipaumbele katika mapambano dhidi ya ugonjwa huu ambao historia yake inaturudisha karne nyingi zilizopita.

Mwaka 2020, jumla ya visa 1,208 vya ukoma viligundulika nchini, ambapo mikoa ya Morogoro, Dar es Salaam na kisiwa cha Unguja iliongoza kwa visa hivi.

Ukoma ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea vya bakteria waitwao Mycobacterium leprae, wanaoshambulia mishipa ya fahamu. Maambukizi ya Ukoma ni kwa njia ya hewa pekee kupitia majimaji kutoka mfumo wa upumuaji wa mtu mwenye maambukizi ya Ukoma akipiga chafya au kukohoa. Tofauti na dhana potofu iliyosambaa kwa jamii nyingi, ugonjwa wa Ukoma hauambukizwi kwa kugusana au kushikana mikono.

Dalili za Ukoma:

  • Vijinundu kwenye ngozi
  • Baka au mabaka mwilini yenye rangi ya shaba yasiyo na hisia
  • Mishipa ya fahamu kuvimba
  • Ganzi kwenye mikono na miguu

Njia pekee ya kujikinga dhidi ya madhara ya Ukoma ni kwa kufanya uchunguzi wa mara kwa mara na utambuzi wa mapema wa dalili zake ili kupata matibabu.

UKOMA UNATIBIKA! Iwapo mgonjwa wa ukoma atagundulika mapema, atapata matibabu ya dawa na kupona kabisa.

Tangu kuanzishwa kwa ugawaji wa dawa tiba za Ukoma kupitia Mpango wa Taifa wa Kifua Kikuu na Ukoma(NTLP) kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani(WHO), visa vya ukoma nchini vimepungua kutoka visa 35,000 mnamo mwaka 1983 hadi kufikia takribani visa 1,200 mwaka 2020.

Madhara ya Ukoma:

  • Misuli kukosa nguvu
  • Kupooza
  • Matatizo ya macho na kupelekea upofu
  • Ulemavu wa mikono na miguu

Kutokana na madhara ya Ukoma, waathirika wengi wa ugonjwa huu hunyanyapaliwa na kutengwa na jamii kwa hofu ya kuambukiza wengine. Tunapoadimisha Siku ya Ukoma Duniani, nitoe wito kwa jamii kuepuka kuwanyanyapaa waathirika wa ugonjwa huu na kuendelea kuchukua tahadhari. Iwapo utaona dalili mojawapo, wahi katika kituo cha kutolea huduma za afya kilicho karibu nawe kwa matibabu zaidi.

Sources: NTLP, Wizara ya Afya, WHO Tanzania